Mkuu wa Wilaya ya Liwale, Mheshimiwa Goodluck Mlinga, amefungua rasmi semina kwa vikundi maalumu vinavyotarajia kunufaika na mikopo ya asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Liwale inayotolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Semina hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Tengeneza, ikiwa na lengo la kuwajengea uwezo wanavikundi kuhusu taratibu, matumizi na marejesho ya mikopo hiyo.
Akizungumza wakati wa ufunguzi, Mheshimiwa Mlinga amewapongeza wananchi wa Liwale kwa kudumisha amani na utulivu wakati wa uchaguzi uliopita na kuwataka kutumia fursa zilizopo kujiletea maendeleo. Amesisitiza umuhimu wa kutumia mikopo hiyo kwa uadilifu, kuhakikisha inarejeshwa kwa wakati ili vikundi vingine navyo viweze kunufaika. Aidha, ameziagiza kamati za kata kuhakikisha mikopo inatolewa kwa walengwa halali, miradi inaendeshwa kwa tija, na marejesho yanafanyika kwa muda uliopangwa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii Halmashauri ya Wilaya ya Liwale, Bw. Hamis Namaleche, ameeleza kuwa kwa mwaka wa fedha 2024/2025 jumla ya Shilingi 773,523,370 zilitolewa kwa vikundi 201, huku Shilingi 238,700,954 zikiwa zimekusanywa kama marejesho. Amesema kwa robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026, jumla ya vikundi 57 kati ya 324 vilivyowasilisha maombi vimepitishwa, vikiwemo vikundi 32 vya wanawake, 21 vya vijana na 4 vya watu wenye ulemavu, ambavyo vitapata mikopo yenye thamani ya Shilingi 308,581,300.
Bw. Namaleche ameongeza kuwa shughuli kuu zinazotekelezwa na wanufaika ni usafiri na usafirishaji, mama lishe, ushonaji na biashara mchanganyiko. Hata hivyo, amebainisha kuwa baadhi ya vikundi havikupata mikopo kutokana na kukosa sifa, ikiwemo kuwa na wanachama waliostaafu, kutokuwa na leseni za udereva kwa vikundi vya usafirishaji, au kuwa na wanachama wanaotoka nje ya kata husika. Aidha, alikumbusha kuwa kikundi kinatakiwa kuwa na angalau wanachama watano wanaokamilisha masharti yote kabla ya kuidhinishwa kupata mkopo.
Along Nachingwea Road opposite DDD Quarters
Sanduku la Posta: P.O. BOX 23 LIWALE
Simu ya Mezani: 023 2937043
Mawasiliano ya mkononi:
Baruapepe: ded@liwaledc.go.tz
Hakimiliki 2023 © Halmashauri ya Wilaya ya Liwale. Haki zote zimehifadhiwa.